Leo Ijumaa Tarehe 14/04/2023 Baraza la mitihani Tanzania(NECTA) limehitimisha mafunzo ya siku mbili kuhusu mfumo wa kielektroniki wa utunzaji wa taarifa za wanafunzi(PReM), kwa walimu wa shule za msingi Halmashauri ya Mji Handeni. Katika mafunzo hayo mada mbalimbali zilifundishwa ikiwemo namna ya kujaza taarifa za wanafunzi, namna ya kufanya uhamisho wa wanafunzi kutoka shule moja Kwenda nyingine pamoja na namna ya kutumia mfumo huo kwa kufuata taratibu zote za kiusalama wa taarifa hizo. Mafunzo hayo yaliyofanyika katika ukumbiwa chuo cha maendeleo ya wananchi FDC yamehudhuriwa na wataalamu mbalimbali kutoka Baraza la mitihani Tanzania(NECTA), Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Handeni, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maafisa Elimu msingi, Maafisa Tehama wa Halmashauri ya Mji Handeni, wakuu wa shule na watakwimu wa shule zote za msingi za Halmashauri ya Mji Handeni
Katika mafunzo hayo ndugu Sadick Manjoti mtaalam wa Tehama kutoka Baraza la mitihani Tanzania(NECTA), amewataka walimu kuchukua tahadharij juu ya usalama wa taarifa za wanafunzi wanazoziweka katika akaunti zao, dhidi ya wadukuzi wa aina tofauti ambao wanaweza kupelekea upotevu na uharibifu wa taarifa au upatikanaji wa taarifa kwa wasiohusika.
Walimu wakuu na watakwimu wa shule za msingi Halmashauri ya Mji Handeni, wakifuatilia kwa makini mafunzo ya mfumo wa utunzaji wa taarifa za wanafunzi(PReM)
Kwa upande wake Bi.Asha Hemedi, Afisa usajili kutoka Baraza la mitihani Tanzania(NECTA), amewataka walimu hao kuhakikisha wanajaza taarifa za wanafunzi mapema ili kuweza kupata muda wakutosha, kupitia upya na kuhakiki taarifa hizo ili kuepusha taarifa zisizosahihi, ambazo huathiri bajeti ya shughuli za uendeshaji wa zoezi la mitihani kwa shule husika.
Mtakwimu wa shule ya msingi Mpakani Mwalimu. Saumu Magongo, akiuliza swali katika mafunzo ya mfumo wa utunzaji wa taarifa za wanafunzi(PReM)
Nae Afisa Elimu msingi wa Halmashauri ya Mji Handeni ndugu Shomari Bane, amewataka walimu kuzingatia muda wa kujaza taarifa za wanafunzi ili kuepusha ucheleweshaji wa taarifa, pamoja na hivyo ndugu Shomari Bane amemshukuru Raisi wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania Dokta. Samia Suluhu Hassan, kuwawezesha walimu kwa kuwapatia vishikwambi, ambavyo vimekuja kutatua changamoto ya uhaba wa vifaa vya Tehama, hivyo wanaweza kutumia mifumo mbalimbali kwa urahisi na kwa wakati husika kutokana na vishikwambi hivyo.
Mheshimiwa.Mussa Mkombati akizungumza na walimu wa shule za msingi Halmashauri ya Mji Handeni, katika mafunzo ya mfumo wa utunzaji wa taarifa za wanafunzi(PReM) yaliyofanyika katika ukumbi wa chuo cha maendeleo ya wananchi (FDC)
Akizungumza na walimu waliohudhuria katika mafunzo hayo Mwnyekiti wa Halmashauri ya Mji Handeni Mheshimiwa.Mussa Mkombati, amewasihi walimu kujiepusha na suala la udanganyifu wa mitihani, kwani serikali ipo makini na haitafumbia macho suala hilo, pia amewataka walimu wajiepushe na udanganyifu katika takwimu za wanafunzi, kuzihakiki upya na kurekebisha pale ambapo zina makosa. Mheshimiwa.Mussa Mkombati amewataka walimu na watendaji wote wa shule kupambana katika kuwezesha wanafunzi kuwa na uwezo wa kujua kusoma, kuandika na kuhesabu, kufuta utoro na kuhakikisha wanafunzi wanapata chakula wakiwa shuleni pia amewasisitiza walimu kushirikiana na viongozi wa serikali za mitaa na kata husika wakati wanapofanya mikutano yao, ambao viongozi hao ndio wasimamizi wakuu wa maadhimio ya mikutano hiyo.
Nae Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni Bi. Maryam Ukwaju, amewasisitiza walimu juu ya kufuata taratibu sahihi za matumizi ya mfumo wa FFARS, ambao ndio mfumo pekee wa ufanyaji malipo ili kuepusha hoja katika kipindi cha ukaguzi, pia amewataka kuzingatia taratibu zote za kuomba fedha za uhamisho kwani ni haki ya kila mtumishi pale anapohamia makazi mapya katika utumishi wake na kujiepusha na tabia za kughushi barua za uhamisho, akihitimisha Bi.Maryam Ukwaju amewataka walimu kusaidiana na wazazi kuwalea watoto katika maadili mazuri ili kudhibiti tatizo la mmomonyoko wa maadili katika Jamii.
Abdulkadir Kassim
Handeni Mji
Barabara ya Korogwe - Handeni
Anuani ya Posta: S.L.P 51 HANDENI
Simu ya Mezani: 027-2641807
Simu ya Mkononi:
Barua pepe: td@handenitc.go.tz
Copyright ©2022 GWF . All rights reserved.